Rais  wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli leo
 asubuhi katika Ikulu ya Dar es Salaam  amefanya kikao na Makatibu 
wakuu, Manaibu Makatibu wakuu, Gavana wa Benki Kuu Prof. Benno Ndulu na 
Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)  ili kutoa uelekeo wa 
Serikali anayoitaka  mara baada ya  kuapishwa.
 
    “Nataka Serikali iendelee kwa nguvu zote na katika kutekeleza dhana 
ya ‘HAPA KAZI TU’ na viongozi kuzingatia na kukumbuka ahadi nilizotoa 
ili zianze kuonekana na kufanyiwa kazi mara moja” Rais Magufuli amesema.
 
    Katika Kikao chake, Rais ametoa mwongozo na kusisitizia kuwa ni 
lazima kila mtendaji Serikalini kuuzingatia, kufuata sheria na taratibu 
ili taifa lisonge mbele kwa ufanisi zaidi. Katika kikao hicho Rais 
ameelekeza mambo kadhaa ambayo watendaji hao wanapaswa kuyasimamia, 
kuyawekea mikakati na kuyapanga vizuri ili atakapo teua Baraza lake la 
Mawaziri mambo hayo yawe tayari ili Mawaziri watakaoteuliwa waweze 
kuyasimamia bila kukosa.
 Mambo hayo muhimu ni kama ifuatavyo:
Kuanzia
 mwezi  Januari mwaka 2016, wanafunzi wote wanaoanza shule watasoma bure
 bila kulipa ada, Katika jambo hili, Rais amewataka watendaji kuanza 
kuliwekea mikakati tayari kwa utekelezaji Suala la mikopo ya wanafunzi 
nalo lifanyiwe kazi na mipango yake ikamilike kwa ajili ya utekelezaji 
mzuri zaidi Amefuta safari zote za nje ya nchi kuanzia leo hadi hapo 
atakapolitolea suala hilo maamuzi mengine na kueleza kuwa shughuli zote 
zinazotakiwa kufanywa nje ya nchi zifanywe na kusimamiwa  na mabalozi wa
 Tanzania  wanaowakilisha nchi  huko nje.
Pengine patokee jambo la dharura sana na hata hilo lazima kibali kitolewe na Rais au Katibu Mkuu Kiongozi. Badala yake Rais amewataka watendaji hao kufanya zaidi ziara za kwenda vijijini ili kuzijua na kutatua kero za wananchi wa Tanzania.
 
    Katika Kikao hicho, Rais amemtaka Kamishna wa TRA, Ndugu Rished Bade
 kusimamia kwa makini zoezi la ukusanyaji wa mapato nchini na 
kuhakikisha kero ndogo ndogo kwa wananchi lianze kutekelezwa kama alivyo
 ahidi kwa  kufanyiwa  kazi mapema  zaidi.
 
    Rais ameitaka TRA kukusanya mapato hayo kutoka kwa wafanya biashara 
wakubwa zaidi na wale wanaokwepa kodi bila kuogopa mtu wala taasisi 
yoyote hapa Tanzania na kusisitiza kuwa katika Serikali hii wa kutoa 
maamuzi vinginevyo zaidi ya haya ni yeye Rais  ama Makamu wake.
 
    Rais Magufuli pia ameagiza usimamizi katika suala la manunuzi ambalo
 limekuwa likitumika vibaya na kuwa mwanya wa kuibia Serikali  kwa watu 
kuongeza bei ya vitu hata kama ni vya bei ndogo kabisa katika jamii.
 
    “Ikitokea suala hilo likagundulika kwa watu kuongeza bei ya vitu, 
watendaji watawajibishwa mara moja”. Rais amesema, na kuwataka watendaji
 hao kufanya kazi zao kwa kuzingatia Sheria na taratibu zilizopo na 
kuzingatia maadili mema ya kazi.
 
 
 
 
 
 

 
 
0 comments:
Post a Comment