Pages

Ads 468x60px

Tuesday, December 15, 2015

CHAMA CHA SANAA CHA TINGATINGA CHATILIANA SAINI MKATABA WA MIAKA MITANO WA KUFANYA KAZI NA KAMPUNI YA BRICOLEUR HOLDINGS YA NCHINI JAPAN

 Mkurugenzi wa Kampuni ya Bricoleur Holdings ya nchini Japan, Bi. Yu Shiran (katikati) akiongea na Waandishi wa Habari (hawapo pichani) kuhusu kushirikiana kufanya kazi za sanaa na Kikundi cha Sanaa cha Tingatinga, leo katika Ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO). Kulia ni Mwenyekiti wa Kikundi cha Sanaa (Tingatinga), Bwana Zachi Chimwanda na kushoto ni Mkurugenzi pia wa Kampuni ya Bricoleur Holdings ya nchini Japan, Bwana Shoji Tsuchiya.
Katibu Mtendaji wa Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), Bwana Godfrey Mngereza (kushoto) akifafanua jambo wakati wa utiaji saini wa Mkataba wa makubaliano kati ya Kikundi cha Sanaa cha Tingatinga na Kampuni ya Kampuni ya Bricoleur Holdings ya nchini Japan. Katikati ni Wakurugenzi wa Kampuni ya Bricoleur Holdings ya nchini Japan Bwana Shoji Tsuchiya pamoja na Bi. Yu Shiran.

Na Tupokigwe Marco na Mwanahamisi Matasi

Chama cha Sanaa cha uchoraji picha maarufu kama Tinga Tinga kimetiliana saini Mkataba wa Makubaliano wa miaka mitano wa kufanya kazi kwa pamoja na Kampuni ya  Bricoleur Holdings Co. Ltd ya nchini Japan utakaokiwezesha chama hicho kunufaika kwa kuuza kazi zake Kimataifa.

Akiongea leo wakati wa utiaji saini wa Mkataba huo, Mwenyekiti wa Chama cha Sanaa cha Tinga Tinga, Bwana Zachi Chimwanda ameeleza kuwa, utiaji saini wa Mkataba huo utakua chachu ya maendeleo katika kuwakomboa wasanii wachoraji katika kipato chao na kuboresha hali zao za kimaisha kwakuwa kazi zao sasa zitakuwa zikiuzwa ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Baraza la Wasanii la Taifa (BASATA), Bwana Godfrey Mngereza alieleza kuwa Mkataba waliosaini kati ya Tinga Tinga na watu wa Bricoleur Holdings Co. Ltd utaimarisha kazi za Wasanii katika fani ya uchoraji ikiwemo kuongeza vipato vyao.

''Sanaa ni kazi lakini pia ni biashara, imefika wakati kwa wasanii kufaidika na jasho lao, kampuni hii watakua wakitafuta masoko kule Japan ili kazi hizi za wachoraji toka Tanzania ziweze kununuliwa hali ambayo itawaongezea kipato'', alisema Mngereza.

Aliongeza kuwa Mkataba uliosainiwa kati ya pande zote mbili umepitia taratibu zote za kiserikali na Taasisi zinazohusika na mambo ya sanaa na maslahi ya msanii na msanii yule aliyehusika katika kuchora picha fulani atanufaika na mkataba huo.

''Kwa msanii atakehusika binafsi na uchoraji picha mkataba utamwezesha kujua atanufaika vipi na kwa muda gani'', aliongeza Mngereza.Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kampuni ya Bricoleur Holdings Co. Ltd, Bi. Yu Shiran ameeleza kuwa mpango huo wa Mkataba kati yao na Tingatinga una lengo la kukitangaza Chama hicho cha wachoraji wa Tanzania Kimataifa.

‘’Kwa kutumia taarifa za kidijiti za Tingatinga tutaweza kushirikiana na watengenezaji mbalimbali wa bidhaa, na ili kulithibitisha hili, sisi na Tingatinga tumekuwa katika mjadala wa takriban mwaka mzima sasa’’, alisema Bi. Shiran.

Tinga Tinga Arts Group lilianzishwa nchini Tanzanja na Edward Saidi Tingatinga ambaye alifariki mwaka 1972 ambapo kwa sasa kundi hilo lipo maeneo ya Oysterbay jijini Dar es Salaam kikijihusisha na sanaa ya uchoraji.

0 comments:

Post a Comment

 
Blogger Templates